Thursday 26 February 2015

Mara baada ya kukufndisha juu ya FUNGUO TANO za kufungua malango na milango, sasa nataka nikufundishe juu ya kipengele kingine ambacho ni ;









SILAHA NANE ZA KUFUNGUA MILANGO NA MALANGO YALIYOFUNGWA MBELE YAKO;

Maombi yetu ya Kufungua Milango na Malango yaliyofungwa inahitaji Uhodari na Uthabiti katika Imani, hivyo lazima silaha hizi zitumike ndipo Milango na Malango yaliyofungwa yatafunguliwa. Kufungua kilichofungwa si kazi rahisi. Maandiko matakatifu yanasema; “Hatimaye mzidi kuwa hodari katika Bwana na katika uweza wa nguvu zake. Vaeni silaha zote za Mungu mpate kuweza kuzipinga hila za shetani; kwa maana kushindana kwetu si juu ya damu na nyama bali ni juu ya falme na mamlaka juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa Roho, kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama.” Waefeso  6:10-14
Maisha yetu ya Kristo yapo katika mgongano wa kiroho na shetani na huu mgongano unaitwa VITA VYA IMANI. Ambavyo vinaendelea hadi atakapokuja mara ya pili Yesu Kristo kuvikomesha. Lakini ushindi wa mtu wa Mungu umehakikishwa na Kristo mwenyewe kwa njia ya kifo chake pale msalabani. Alipokufa na kufufuka ametangaza ushindi kwa kila amwaminiye tangu wakati ule hata sasa tunashinda na zaidi ya kushinda. Palipo na neno “KUSHINDA” maana yake pana neno “KUSHINDANA”.
Maisha yetu ya imani ni ya kushindana na kushinda. Wengine kwa kutokujua, adui alipokuja kushindana nao wakaogopa, wakaona Mungu amewaacha na kujiuliza maswali mengi KWANINI BWANA AMEYARUHUSU HAYA? Kumbe maisha ya ukristo halisi ni vita sio lelemama ndiyo maana BWANA anasema tuwe hodari na moyo wa ushujaa. “Uwe hodari na moyo wa ushujaa, maana ni wewe utakaye warithisha watu hawa… uwe hodari tuu na ushujaa mwingi, uangalie kutenda sawasawa na sheria yote… usiache kwenda mkono wa kuume au wa kushoto, upate kufanikiwa sana kila uendako.” Yoshua 1:6-7
BWANA umtumia mtu hodari na mwenye moyo wa ujasiri sio mtu legelege na dhaifu. Ndiyo maana alimtumia Daudi kumpiga Goliati kwa sababu alikuwa na moyo wa uhodari na ujasiri mwingi. Daudi hakwenda vitani kubahatisha bali alikwenda ksuhindana na kushinda ndivyo ilivyotokea. Maandiko yanasema; “Mtu mwenye nguvu aliyejifunga silaha zake alindapo nyumba yake, vitu vyake vi salama lakini mtu mwenye nguvu kuliko yeye atakapomwendea na kumshinda, amnyang’anya silaha zake zote alizokuwa akizitegemea na kuyagawanya mateka yake.” Luka 11:21-22

Yesu Kristo anahimiza kujifunga silaha zetu na kuyalinda Malango na Milango yetu. Pasipo kujifunga silaha hatuwezi kumshinda yule adui shetani. Lazima uzivae hizi silaha ndipo zitakazofanya Ushinde Falme za giza, Wakuu wa giza hili na kuyashinda Majeshi ya pepo wabaya. Maandiko yanasema; “Maana ingawa tunaenenda katika mwili hatufanyi vita kwa jinsi ya mwili, maana silaha za vita vyetu si za mwili bali zinauwezo katika Mungu hata kuangusha ngome.” 2Wakorinto 10:3-4

Vita vyetu vya kiroho sharti vipiganwe kwa silaha za rohoni – pasipo kuvaa hizi silaha za kiroho hatuwezi kuziangusha ngome zilizojengwa kinyume na zenye kuhakikisha Malango hayafunguliwi.

SILAHA YA KWANZA
Zipo silaha nane za kiimani zenye nguvu za kufungua malango na milango iliyofungwa katika maisha yetu ya kiroho na kimwili. Silaha hizo ni:-

(i) KATAA
    Imani ni kuwa na hakika katika Mungu na mwenye haki ataishi kwa imani. Maandiko matakatifu yanaonyesha waziwazi ya kuwa msingi wa wokovu ni imani. Yatupasa kuyakataa yale tusiyoyaamini katika imani yetu, mfano wa Musa alivyokataa kuitwa mtoto wa binti Farao, japo kuitwa mtoto wa binti Farao kulikuwa na faida nyingi za kimwili lakini akachagua ufalme wa Mungu na haki yake kuliko ufalme wa Farao ambao mwisho wake ni kutupwa jehanamu ya moto. Hivyo Musa akatumia silaha hii ya kwanza ya KUKATAA matokeo yake BWANA akamtumia kama shujaa na mkombozi wa wana wa Israeli toka utumwani Misri. Maandiko matakatifu yanathibitisha; “Kwa Imani Musa alipozaliwa alifichwa miezi mitatu na wazazi wake kwa sababu waliona kwamba ni mtoto mzuri wala hawakuogopa amri ya mfalme KWA IMANI MUSA ALIPOKUWA MTU MZIMA ALIKATAA KUITWA MWANA WA BINTI FARAO. Akaona afadhali kupata mateso kuliko kujifurahisha katika dhambi kwa kitambo akihesabu kushutumiwa kwake Kristo ni UTAJIRI MKUU kuliko hazina za Misri kwa kuwa aliyatazamia hayo malipo. Kwa Imani akatoka Misri, asiogope ghadhabu ya mfalme, maana alistahimili kama amuonaye yeye asiyeonekana kwa Imani alifanya Pasaka, na kule kunyunyiza damu ili yule mwenye kuangamiza wazaliwa wa kwanza asiwaguse wao” Waebrania 11:23-28

Musa alikataa kuitwa mtoto wa binti Farao, ukawa ndio mlango wa ukombozi wa wana wa Israel kutoka katika milango ya kuzimu ya Farao. Hii ni silaha kubwa sana ambayo lazima tuivae kabla ya mambo yote. Ni lazima kwa Moyo wako wote na Roho yako yote na kwa Akili zako zote Kataa hali uliyonayo katika ulimwengu wa Roho ama katika Mwili. Maandiko matakatifu yanasema; “Tumbo la mtu litajazwa matunda ya kinywa chake; Atashiba mazao ya midomo yake. Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi; Na wao waupendao watakula matunda yake.” Mithali 18:20-21
Ukiri katika ulimi una nguvu ya kuangusha malango na milango ya kuzimu hivyo ulimi wa imani ni mti wa uzima. Ni vema kutumia ndimi zetu kujitamkia mema sisi wenyewe, kutamka mema kwa watoto wetu na juu ya mali zetu maana BWANA Mungu alitamka iwe na ikawa. “Ulimi wa mwenye haki ni kama fedha teule; Moyo wa mtu mbaya haufai kitu” Mithali 10:20

Dada mmoja pale Morogoro eneo la Forest aliokoka akiwa na miaka kumi na mitano (Miaka 15), siku moja akiwa anatoka shule pale Morogoro mjini, alikutana na mvulana mmoja kumbe ni mjumbe wa shetani (mtu jini) lakini yeye aliona ni mvulana, wakasalimiana, lakini kumbe huyu binti amevamiwa na nguvu za yule jinni kwa sababu alimwambia dada nimekupenda naye akasema asante kama utani lakini ndo ukiri wa kinywa. Baada ya hapo huyu binti alianza kuota ndoto mbaya, anafanya mapenzi; hiyo hali iliendelea kwa muda mrefu akiwa ndani ya wokovu. Huyu binti alipokuwa anakuja kwangu kuniona alikuwa na umri wa miaka thelathini na sita (Miaka 36) akiwa bado hajaolewa, hiyo ilikuwa mwaka 2012, akisema;“Mchungaji nimefunga na kuomba na nimetoa sadaka sana lakini sipati mpenyo, ee Mtu wa Mungu niombee.”

Wakati naanza kumpa ushauri ili nipate kumwombea, nikaitiisha ile nguvu iliyo mfunga kwa jina lenye nguvu la Yesu Kristo. Ndipo nguvu ya pepo jinni dume likapiga kelele likidai huyu binti ni mke wake, limemuoa akiwa na umri wa miaka kumi na mitano kule Morogoro. Nikaipinga ile nguvu ya pepo, nikasema huyu ameokoka, ninyi mnawezaje kukaa ndani yake? Nikahoji tena ni mlango  gani mliotumia kumfunga huyu binti; yule jini akasema waziwazi huyu binti ni mvumilivu na mwaminifu sana kwa huyo Mungu wenu, lakini mimi ninammiliki kwa sababu yeye mwenyewe hajawahi kunikataa na kuitengua ndoa yetu, kwani hujui imeandikwaje katika Warumi? “Kwasababu ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, Utaokoka. Kwa maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu.” Warumi 10:9-10

Yule kijana (Jini) alimwambia binti nakupenda naye akakubali lakini hawakuonana tena na ni miaka zaidi ya kumi na sita ndoa ipo katika ulimwengu wa roho. Ukiri una nguvu ya Uzima ama Mauti. Ni lazima ukatae  na utengue kila mkataba na maagano yote ya giza sawasawa na kuamini kwako. Ndiyo maana Musa alikataa kwanza kabla ya wito wake. Tendo la kukataa kuitwa binti Farao ndilo likamfanya Mungu amuite kwa kazi yake.

Wakristo wengi wanataka kufunguliwa Milango na Malango lakini bado hawajakataa kabisa Mizimu ya ukoo, Mizimu ya mababu na mabibi zao, maagano mbalimbali walioungamanishwa kwayo kabla ya wokovu. Usikiri Udhaifu juu yako, juu ya watoto wako, juu ya mume wako, juu ya mke wako, juu ya kazi yako, juu ya ndoa yako wala juu ya maisha yako.
         
 “Neno BWANA lilinijia, kusema, kabla sijakuumba katika tumbo nalikujua, na kabla hujatoka tumboni, nalikutakasa; Nimekuweka kuwa nabii wa mataifa. Ndipo niliposema, Aa, Bwana Mungu! Tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto. LAKINI BWANA akaniambia, USISEME, Mimi ni mtoto maana utakwenda kwa kila nitakayekutuma kwake, nawe UTASEMA KILA NENO NITAKALOKUAMURU. Usiogope kwasababu ya hao maana mimi nipo pamoja nawe nikuokoe, asema Bwana” Yeremia 1:4-8

Usiseme kinyume na Neno la Mungu juu yako maana BWANA anakuwazia mema naye ulituma Neno kwako lipate kukuponya na kukufungulia milango na malango ya Baraka na Ustawi.
Angalia Musa pamoja na BWANA kumtumia katika kutenda maajabu na miujiza mingi, lakini Musa alikufa akiwa na  utasi (kigugumizi) kwa sababu hakuukataa udhaifu huo bali aliukubali kuwa sehemu ya maisha yake. Maandiko yanathibitisha;
“Musa akamwambia BWANA, Ee Bwana, mimi si msemaji tokea zamani, wala tokea hapo uliposema na mtumishi wako; maana mimi si mwepesi wa kusema, na ulimi wangu ni mzito. Bwana akamwambia, Ni nani aliyekifanya kinywa cha mwanadamu? Au ni nani afanyaye mtu kuwa bubu au kiziwi, au mwenye kuona, au kuwa kipofu? Si mimi, BWANA? Basi sasa, enenda, nami nitakuwa pamoja na kinywa chako, na kukufundisha utakalolinena. Akasema, Ee Bwana nakuomba, tuma kwa mkono wake huyo utakayemtuma. HASIRA YA BWANA ikawaka juu ya Musa, akasema, je! Hayuko Haruni, ndugu yako, Mlawi? Najua ya kuwa yeye aweza kusema vizuri. Pamoja na hayo, tazama, anakuja kukulaki, naye atakapokuona, atafurahi moyoni mwake. Nawe utasema naye, na kuyatia maneno kinywani mwake; nami nitakuwa pamoja na kinywa chako, na pamoja na kinywa chake, na kuwafundisheni mtakayofanya. Naye atakuwa msemaji wako kwa watu, hata yeye atakuwa mfano wa kinywa kwako, nawe utakuwa mfano wa Mungu kwake. Nawe utatwaa fimbo hii mkononi mwako, na kwa hiyo utazifanya zile ishara.” Kutoka 4:10-17

Mungu alimkasirikia Musa kwa kitendo cha kukataa Uponyaji wa kinywa chake. Matokeo yake mtumishi wa Mungu Musa mpaka anakufa, alikufa akiwa na utasi (kigugumizi).

Pia tunajifunza kwa YABESI; alikataa maisha ya huzuni, Bwana akageuza huzuni zake kuwa heshima. Kabla ya kupokea hicho unachotaka lazima uvae Silaha hii ya kukataa utaona mlango unafunguka mbele yako.“Naye Yabesi alikuwa mwenye heshima kuliko nduguze, na mamaye akamwita jina lake Yabesi, akasema, Ni kwasababu nalimzaa kwa huzuni. Huyo Yabesi akamlingana Mungu wa Israeli, akasema, Lau kwamba ungenibarikia kwelikweli, na kunizidishia hozi yangu na mkono wako ungekuwa pamoja nami, nawe ungenilinda na uovu, ili usiwe kwa huzuni yangu! Naye Mungu akamjalia hayo aliyoyaomba.” 1Nyakati 4:9-11

Pamoja na jina lake kuitwa huzuni, Yabesi alipomjua Mungu alikataa kuitwa huzuni, akakataa maisha ya huzuni. Ndani mwa Maombi haya ya Kufungua Milango na Malango ni lazima tukatae malango yote yaliyotupwa juu yetu au tumezaliwa nayo, maana katika ukiri wa Imani mna nguvu ya kufungua Milango na Malango.

Tunajifunza kwa AYUBU; Pamoja na mateso ya zaidi ya miaka kumi na saba (miaka 17), Kuugua, Kufilisika na Misiba, lakini bado mtumishi huyu wa Mungu alikataa kutamka kinyume cha Imani yake katika Mungu. Katika mambo yote Ayubu hakufanya dhambi wala kumuwazia Mungu kwa upumbavu. “Lakini mimi najua ya kuwa Mteteaji wangu yu hai, Na yakuwa hatimaye atasimama juu ya nchi. Na baada  ya ngozi yangu kuharibiwa hivi. Lakini, pasipokua na mwili wangu nitamuona Mungu; Nami nitamuona mimi nafsi yangu, Na macho yangu yatamtazama, wala si mwingine, Mtima wangu unazimia ndani yangu.” Ayubu 19:25-27

Haya maneno yalifungua Mlango na Milango ya Ayubu tena akainuliwa toka kwenye shimo la uharibifu.  Baada ya hayo yote, BWANA aligeuza uteka wa Ayubu.

 “Basi huyo BWANA akaubarikia mwisho wa Ayubu zaidi ya mwanzo wake, naye alikuwa na kondoo kumi na nne elfu, na ngamia efu sita, na jozi za ng’ombe elfu, na punda wake elfu. Tena alikuwa na wana waume saba, binti watatu. Akamwita huyo wa kwanza jina lake Yemima; na wa pili akamwita jina lake Kesia; na wa tatu akamwita jina lake Keren-hapuhu. Katika nchi hiyo yote hawakuwapo wanawake waliokuwa wazuri kama hao wa Ayubu; na baba yao akawapa urithi kati ya ndugu zao wana waume. Kisha baada ya mambo hayo Ayubu akaishi miaka mia na arobaini, nae akawaona wanawe, na wana wa wanawe, hata vizazi vinne. Basi Ayubu akafa, mzee sana mwenye kujawa na siku.” Ayubu 42:12-16

Ayubu alikataa  Kukiri udhaifu, Kukiri misiba, Kukiri mateso japo alikua kwenye mateso. Alisema, nalitoka tumboni kwa mama yangu ni uchi nitarudi nikiwa uchi. Maandiko matakatifu yanasema; “Maana mwenye kuangalia upepo hatapanda; Naye ayatazamaye mawingu hatavuna. Kama vile wewe usipojua njia ya upepo ni ipi, wala jinsi mifupa ikuavyo tumboni mwake mja mzito; kadharika huijui kazi ya Mungu, afanyaye mambo yote.” Muhubiri 11:4-5

Kwa imani katika Kristo Yesu yatupasa kukataa yaliyokinyume na imani na tukiri yakuwa anaweza kufanya mambo yote;  Aweza Kufungua Milango na Malango yaliyofungwa. Bwana Yesu Kristo anamtumia mtu aliye tayari kutumika na si vinginevyo. Acha kujiua kwa maneno ya kinywa chako. Maana yeye Kristo Yesu ni mwaminifu. Vaa na ujifunge SILAHA yako itakusaidia. “Basi atukuzwe yeye awezaye kufanya mambo ya ajabu mno kuliko yote tuyaombayo au tuyawazayo kwa kadri ya nguvu itendayo kazi ndani yetu.” Waebrania 3:20









UFUNGUO WA TANO

NGUVU ZA ROHO MTAKATIFU

Neno “Nguvu” kwa lugha ya Kigiriki ni (dunamis) ina maana ya zaidi ya Nguvu au Uwezo wa kawaida. “Inaashiria hasa nguvu iliyo katika utendaji wa ki-Mungu, hii ni nguvu zaidi ya nguvu.
(Dunamis is not just any power; it is miraculous power or marvelous works. Dunamis can also refer to “Moral power and excellence of soul according to the Greek lexicon). Nguvu ya Roho mtakatifu inajumuisha mamlaka ya kutoa pepo wachafu na upako wa kuponya magonjwa. Roho mtakatifu ndiye ufunguo wa kumshinda adui shetani na kazi zake. Roho mtakatifu ni zaidi ya nguvu ama uweza. Katika maandiko matakatifu, Yesu kristo alionyesha unafsi wa Roho mtakatifu kwa kumwongelea kama nafsi ambapo alisema; “Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho  wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote; kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake.” Yohana 16:13

Kimsimgi tunajifunza kwa Yesu Kristo kabla ya kuanza huduma yake hapa ulimwenguni, alipokwisha kubatizwa na Yohana mbatizaji, wakati anaomba mbingu zilifunguka Roho mtakatifu akashuka juu yake kwa Nguvu tangia hapo maandiko matakatifu yanathibitisha “Ikawa watu wote walipokwisha kubatizwa, na Yesu naye amebatizwa, naye anaomba, mbingu zilifunuka; Roho mtakatifu akashuka juu yake kwa mfano wa kiwiliwili, kama hua, sauti ikatoka mbinguni wewe ndiye mwanangu mpendwa wangu ninyependezwa nawe.” Luka 3:21-22

Tunajifunza katika maandiko haya yakuwa Nguvu ya Roho mtakatifu haishuki kwa mtu hivihivi mpaka awe anaomba. Lakini wako wakristo wengi wanaotaka kujazwa Roho mtakatifu wakati hawana maombi katika maisha yao. Maombi ufungua mbingu zimfungukie mwombaji. Baada ya Yesu kristo kujazwa Roho mtakatifu, maandiko matakatifu yanashuhudia wazi yakuwa aliongozwa na Roho muda wa siku arobaini katika maombi. “Naye Yesu, hali amejaa Roho mtakatifu, alirudi kutoka Yordani, akaongozwa na Roho muda wa siku arobaini nyikani.”  Luka 4:1

Pia yunajifunza ili milango na malago ya ukombozi wa mwanadamu yapate kufunguliwa ilibidi Roho mtakatifu ashuke kwa nguvu na uweza mkuu ili kumfunika mwanamwali bikra apate uwezo wa kubeba mimba pasipo kukutana na mwanamume kwa jinsi ya kibinadamu.
“Mwezi wa sita, malaika Gabrieli alitumwa na Mungu kwenda mpaka mji wa Galilaya, jina lake Nazareti, kwa mwanamwali bikira aliyekuwa ameposwa na mtu, jina lake Yusufu, wa mbari ya Daudi; na jina lake bikira huyo ni Mariamu. Akaingia nyumbani kwake akasema, Salamu, uliyepewa neema, Bwana yu pamoja nawe. Naye akafadhaika sana kwa ajili ya maneno yake, akawaza moyoni, Salamu hii ni ya namna gani? Malaika akamwambia, Usiogope, Mariamu, kwa maana umepata neema kwa Mungu. Tazama utachukua mimba na kuzaa mtoto mwanamume, na jina lake utamwita Yesu. Huyo atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa aliye juu, na Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake. Ataimiliki nyumba ya Yakobo hata milele, na ufalme wake utakuwa hauna mwisho. Mariamu akamwambia malaika, Litakuwaje neno hili, maana sijui mume? Malaika akajibu akamwambia, ROHO MTAKATIFU ATAKUJILIA JUU YAKO, na nguvu zake aliye juu zitakufunika kama kivuli; kwa sababu ya hicho kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, mwana wa Mungu.”

Roho mtakatifu akishuka kwetu huja na nguvu zake aliye juu katika Uwezo na nguvu za Roho Mtakatifu, tunavishwa uwezo wa kuangusha ngome zote zilizofunga Malango na Milango yetu ya Baraka za kiroho na kimwili, ndiyo maana Bwana Yesu kristo alisema, Mtapokea nguvu akisha kuwajilia Roho Mtakatifu. Mkristo nguvu yako haimo katika vitu vya upako kama vile; mafuta ya upako, maji ya upako, sabuni za upako, chumvi ya upako, kitambaa cha upako, udongo wa upako, kiganja cha nabii wa upako nambo yafananayo na hayo yanayoibuliwa kila kukicha katika ibada zilizotungwa kwa akili za binadamu. Ndugu mpendwa katika kristo yachunguzeni maandiko vema; mpate kuijua kweli inayoweza kuwawekeni huru mbali na mateso. Tukiwa na msimamo thabiti wa kiimani yatupasa kuliamini Neno la Mungu sio maneno ya watu, watawaijieni kwa mfano wa wanakondoo lakini ndani ni mbwa mwitu wakali. Maagizo ya Yesu Kristo aliye mwanzilishi wa huduma hii iliyokubwa na bora anasema;  Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.” Matendo 1:8
Yesu kristo aliwaambia wanafunzi wake msitoke Yerusalemu bali mwingojee nguvu ya Roho mtakatifu, ambayo kwa hiyo watatenda kazi ya kufungua waliofungwa. Maana pasipo huyo Roho mtakatifu hakuna atakayeweza. Tunaona akina Petro na Yohana baada ya kupokea Nguvu ya Roho mtakatifu waliweza kunena habari za Kristo Yesu na ufalme wake kwa ujasiri na nguvu. Hata wengi walistaajabu walipoona ujasiri wao. “Ndipo Petro akijaa Roho mtakatifu, akawaambia, enyi wakubwa wa watu na wazee wa Israeli … wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine katika mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo. Basi walipoona ujasiri wa Petro na Yohana, na wakajua ya kuwa ni watu wasio na elimu, wasio na maarifa wakastaajabu wakatambua ya kwamba walikuwa pamoja na Yesu.” Mdo 4:8-13

Kwa hiyo Roho mtakatifu akiwa kwa mtu hujidhihirisha kwa madhihiriho ya ishara, miujiza na maajabu ambayo huwastaajabisha wengi wayaonapo. Roho mtakatifu uhuisha nafsi zetu na miili yetu toka kwenye mafungo ya giza kwa kutufungulia malango na milango. Tunajifunza kwa Lazaro alipougua, akafa, akazikwa kwa muda wa siku nne alikuwamo kaburini lakini kwa nguvu za Roho mtakatifu Yesu alipaza sauti yake akamwita Lazaro toka kwa wafu akawa hai tena. Hata sasa Roho mtakatifu bado anatenda kazi kwa wote waaminio maana tukimwita katika Kristo Yesu ushuka kuokoa na kuponya wengi. Hata kama lipo kaburi limefunga maisha yako ya kiroho na kimwili kwa uweza na nguvu za Roho mtakatifu sharti ufunguliwe. (Through Power of Holy Ghost we Force out evil spirit). Maandiko yanasema katika injili ya Yohana;Basi mtu mmoja alikuwa hawezi, Lazaro wa Bethania, mwenyeji wa mji wa Mariamu na Martha, dada yake. Ndie Mariamu yule aliyempaka Bwana marhamu, akamfuta miguu kwa nywele zake, ambaye Lazaro nduguye alikuwa hawezi. Basi wale waumbu wakatuma ujumbe kwake wakisema, Bwana, yeye umpendaye hawezi. Naye Yesu aliposikia, alisema, Ugonjwa huu si wa mauti, bali ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu, ili mwana wa Mungu atukuzwe kwa huo. Naye Yesu alim,penda Martha na umbu lake na Lazaro. Basi aliposikia ya kwamba hawezi, alikaa bado siku mbili pale pale alipokuwapo. Kisha, baada ya hayo, akawaambia wanafunzi wake, Twendeni Uyahudi tena. Wale wanafunzi wakamwambia, Rabi, juzi juzi tu Wayahudi walikuwa wakitafuta kukupiga kwa mawe, nawe unakwenda huko tena? Yesu akajibu, Je! Saa za mchana si kumi na mbili? Mtu akienda mchana hajikwai; kwa sababu aiona nuru ya ulimwengu huu. Bali akienda usiku hujikwaa; kwa sababu nuru haimo ndani yake. Aliyasema hayo; kisha baada ya hayo, akawaambia, Rafiki yrtu, Lazaro amelala, lakini ninakwenda nipate kumwamsha. Basi wale wanafunzi wakamwambia, Bwana, ikiwa amelala, atapona. Lakini Yesu alikuwa amenena habari ya mauti yake; nao walidhania ya kuwa ananena habari ya kulala usingizi. Basi hapo Yesu akawaambia waziwazi, Lazaro amekufa. Nami nafurahi kwa ajili yenu kwamba sikuwako huko, ili mpate kuamini; lakini na twendeni kwake. Basi Tomaso, aitwaye pacha, akawaambia wanafunzi wenziwe, twendeni na sisi, ili tufe pamoja naye. Basi Yesu alipofika, alimkuta amekwisha kuwamo kaburini yapata siku nne. Na Bethania ilikuwa karibu na Yerusalemu, kadri ya maili mbili hivi, na watu wengi katika Wayahudi walikuwa wamekuja kwa Martha na Mariamu, ili kuwafariji kwa habari ya ndugu yao. Basi Martha aliposikia kwamba yesu anakuja, alikwenda kumlaki, na mariamu alikuwa akikaa nyumbani. Basi Martha akamwambia Yesu, bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. Lakini hata sasa najua ya kuwa yo yote utakayomwomba Mungu, Mungu atakupa. Yesu akamwambia, ndugu yako atafufuka. Martha akamwambia, najua yakuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho. Yesu akamwambia, mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi, naye kila aishie na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je! Unayasadiki hayo? Akamwambia, Naam, Bwana, mimi nimesadiki ya kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimmwenguni. Naye alipokwisha kusema hayo, alikwenda zake, akamwita umbu lake Mariamu faraghani, akasema, Mwalimu yupo anakuita. Naye aliposikia aliondoka upesi, akamwendea. Na Yesu alikuwa hajafika ndani ya kijiji, lakini alikuwa akalipo palepale alipomlaki Martha. Basi wale Wayahudi waliokuwapo na Mariamu nyumbani, wamfariji, walipomwona jinsi alivyoondoka upesi na kutoka, walimfuata, huku wakidhani ya kuwa wanakwenda kaburini ili alie huko. Basi Mariamu alipofika pale alipokuwapo Yesu, na kumwona, alianguka miguuni pake, akamwambia, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. Basi Yesu alipomwona analia, na wale Wayahudi waliofuatana naye wanalia, aliugua rohoni, akafadhaika roho yake, akasema, Mmemweka wapi? Wakamwambia, Bwana, njoo utazame. Yesu akalia machozi. Basi Wayahudi wakasema, angalieni jinsi alivyompenda. Bali wengine wao wakasema, je! Huyu aliyemfumbua macho yule kipofu, hakuweza kumfanya na huyu asife? Basi Yesu, hali akiugua tena nafsini mwake, akafika kwenye kaburi. Nalo lilikuwa ni pango, na jiwe limewekwa juu yake. Yesu akasema, Liondoeni jiwe. Martha, dada yake yule aliyefariki, akamwambia, Bwana, ananuka sasa; maana amekuwa maiti siku nne. Yesu akamwambia, Mimi sikukuambia ya kwamba ukiamini utauona utukufu wa Mungu? Basi wakaliondoa lile jiwe. Yesu akainua macho yake juu, akasema, baba, nakushukuru kwakuwa umenisikia. Name nalijua ya kuwa wewe wanisikia siku zote; lakini kwa ajili ya mkutano huu wanaohudhuria nalisema haya, ili wapate kukusadiki kwamba ndiwe uliyenituma. Naye akiisha kusema hayo, akalia kwa sauti kuu, Lazaro, njoo huku nje. Akatoka nje yule aliyekufa, amefungwa sanda miguuni na mikononi, na uso wake amefungwa leso. Naye Yesu akawaambia, Mfungueni, mkamwache aende zake.” Yohana 11:1-44
Roho mtakatifu huleta uzima badala ya mauti; akatoka nje maana yake, akahuwishwa Lazaro toka kwa wafu japo alikuwa amekufa na ameoza. Ijapokuwa alikuwa ananuka, nguvu ya Roho Mtakatifu iliposhuka juu yake aliyekuwa katika hali ya kufa ikamwinua Lazaro toka kwa wafu akawa hai tena. Ni vema kila mmoja aliyeamini kutambua kuwa Roho mtakatifu ni Ufunguo unaotoa nafsi nyingi katika mafungo ya giza. Kwa nguvu za Roho mtakatifu hata kazi zetu za kimwili zaweza kuhuishwa inaweza kuwa Biashara, Kazi, Elimu vyote vilivyozikwa na kufishwa kuwa hai tena. Kama BWANA alivyonena kwa kinywa cha nabii Ezekieli na kusema; “Nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi BWANA, nitakapoyafunua makaburi yenu, na kuwatoa ninyi katika makaburi yenu, enyi watu wangu. Nami nitatia roho yangu ndani yenu, nanyi mtaishi, nami nitawawekeni katika nchi yenu, nanyi mtajua ya kuwa mimi, BWANA, nimesema hayo, na kuyatimiza, asema BWANA.” Ezekieli 37:13-14

Kwa nguvu za Roho mtakatifu sharti malango na milango vifunguliwe ndani mwa maombi sio nje ya maombi kwa kuwa tunapomlilia Mungu na kumwita, yeye hushuka na kutufungua mafungo yetu yote. “Naye Yesu akiisha kupaza sauti tena kwa nguvu, akaitoa roho yake. Na tazama pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu hata chini, nchi ikatetemeka; miamba ikapasuka, makaburi yakafunuka; ikainuka miili mingi ya watakatifu waliolala, nao wakiisha kutoka makaburini mwao, baada ya kufufuka kwake, wakauingia mji mtakatifu, wakawatokea wengi.” Mathayo  27:50-57

Nchi ilitetemeka
Wakuu wa anga lazima watetemeke maana Roho Mtakatifu ni nguvu iliyo juu ya yote lazima Wakuu wa nchi washushwe, Wakuu wa giza washushwe, Wakuu wa majini washushwe katika viti vyao kwani Kila goti lazima lipigwe mbele ya Kristo Yesu Mwokozi. 

Miamba ilipasuka
Wako watu wamefungwa nafsi zao katika miamba na majabali mazito, lazima ipasuke ili wote waachiliwe waliofungwa vifungo kwenye miamba kupitia nguvu ya Roho mtakatifu.

Makaburi yakafunuliwa
Kaburi ni kifuniko kibaya sana kinachotesa wengi. Wengi wanafunikwa makaburini kupitia makafara ya tambiko. Kwa nguvu za Roho Mtakatifu miili mingi ya watakatifu waliofungwa na nguvu ya kaburi watainuka.

Kama pazia la hekalu lilivyopasuka, ndivyo kila kizuizi kilichowekwa katika maisha yako ya kiroho na kimwili kitapasuka toka juu mpaka chini. Huu ndio ulikuwa mwisho wa Agano la kale na kuwa mwanzo wa Agano jipya. Katika Kristo Yesu yakale sasa yamepita tazama yamekuwa mapya. Katika ulimwengu wa Roho watu wengi wamefungwa na mapazia ya mabibi na mababu zao, mapazia ya kiganga na kichawi, mapazia ya mizimu na matambiko, lazima tuwafungue watu wa Mungu mapazia hayo ndani mwa maombi haya ya kufungua milango na malango. Yesu akasema mfungueni sanda mwache aende zake. Ikiwa na maana Lazaro alipofufuka alitoka kaburini akiwa amevaa sanda (vazi la wafu) ndiyo maana Kristo Yesu aliagiza avuliwe hilo vazi yaani sanda ndipo aachwe huru aende zake. Hapa tunapata siri nzito ya kiroho ya kuwa wako wakristo wengi waliookolewa toka katika mafungo ya giza lakini hawajahamishwa na kuingizwa katika ufalme wa mwana wa pendo lake. Ni jukumu letu watumishi wa Mungu kufanya maombi na maombezi ya kuwafungua watu baada ya kuamini. Maana KWELI ya Mungu kupitia Neno ndiyo inayomuweka mtu huru mbali na mateso. Ni muhimu sana tukafundisha na kuombea sawasawa na Neno la Mungu. Maana wako wanaodhania ya kuwa baada ya kuokoka vita vyao vimeisha kumbe wokovu ndio mwanzo wa vita vya kiroho na kimwili. Kwa mantiki hiyo ndiyo maana Bwana Yesu akawaambia wanafunzi wake; “Kesheni mwombe, msije mkaingia majaribuni, roho i radhi ila mwili ni dhaifu.”  Marko 14:38

Hata wana wa Israaeli walipokwisha kuokolewa toka utumwani Misri kwa nguvu na uweza mkuu, tunajifunza kwao jinsi walivyokutana na vipingamizi ambavyo viliwafanya wamlilie Mungu na kupigana vita. Walipigana kiroho, wakapigana kimwili. Mfano halisi ni vita vyao na Waamaleki “Wakati huo Waamaleki wakatokea, wakapigana na Israeli huko Refidimu. Musa akamwambia Yoshua, tuchagulie watu, ukatoke upigane upigane na Waamaleki; kesho nitasimama juu ya kilele kile, na ile fimbo ya Mungu nitakuwa nayo mkononi mwangu. Basi Yoshua akafanya kama Musa alivyomwambia, akapigana na Amaleki; na Musa na Haruni na Huri wakapanda juu ya kile kilima. Ikawa, Musa alipoinua mkono wake, Israeli waliposhinda; na aliposhusha mkono wake, Amaleki walishinda. Lakini mikono ya Musa ilikuwa mizito; basi wakatwaa jiwe, wakaliweka chini yake akalikalia. Haruni na Huri wakaitegemeza mikono yake, mmoja upande huu na mmoja upande huu; mikono yake ikathibitika hata jua lilipokuchwa. Yoshua akawaangamiza Amaleki na watu wake kwa ukali wa upanga. BWANA akamwambia Musa, Andika habari hii katika kitabu iwe ukumbusho, kisha ihubiri masikioni mwa Yoshua; ya kuwa nitaufuta ukumbusho wa Amaleki kabisa, usiwe tena chini ya mbingu. Musa akajenga madhabahu, akaiita jina lake Yehova-nisi; akasema, BWANA ameapa; BWANA atakuwa na vita na Amaleki kizazi baada ya kizazi.”  Kutoka 17:8-16

Wanadamu kwa jinsi ya ubinadamu wao wanaweza kufanya jitihada zao za kiganga na kichawi au za kawaida katika mwili wakakuwekea vipingamizi ili wewe mtu wa Mungu usiinuke. Lakini katika nguvu za Roho mtakatifu tutashinda na zaidi ya kushinda. Angalia mfano, Yesu Kristo walijaribu kumzuia asifufuke toka kaburini kwa kulilinda kaburi kwa kutumia askari wenye silaha na kuweka jiwe kubwa juu ya kaburi. “Hata siku ya pili, ndiyo iliyo baada ya Maandalio, wakuu wa makuhani, na Mafarisayo wakamkusanyikia Pilato, wakasema, Bwana, tumekumbuka kwamba yule mjanja alisema, alipokuwa akali hai, Baada ya siku tatu nitafufuka. Basi amuru kwamba kaburi lilindwe salama hata siku ya tatu; wasije wanafunzi wake wakamiba, na kuwaambia watu, amefufuka katika wafu, na udanganyifu wa mwisho utapita ule wa kwanza. Pilato akaawaambia, mna askari, nendeni mkalilinde salama kadiri mjuavyo. Wakaenda, wakalilinnda kaburi salama, kwa kulitia lile jiwe muhuri, pamoja na wale askari walinzi.” Mathayo 27:62-66
Lakini ilipofika saa ya Roho mtakatifu kudhihirisha nguvu zake, walinzi pamoja na silaha zao walikuwa kama wafu. Maandiko yanathibitisha; “Hata sabato ilipokwisha, ikapambazuka siku ya kwanza ya juma, mariamu Magdalene, na Mariamu yule wa pili, walikwenda kulitazama kaburi. Na tazama, palikuwa na tetemeko kubwa la nchi, kwa sababu malaika wa Bwana alishuka kutoka mbinguni, akaja akaliviringisha lile jiwe akalikalia. Na sura yake ilikuwa kama umeme na mavazi yake meupe kama theluji. Na kwa kumwogopa, wale walinzi wakatetemeka, wakawa kama wafu. Malaika akajibu, akawaambia wale wanawake, Msiogope ninyi, kwa maana najua ya kuwa mnamtafuta Yesu aliyesulibiwa. Hayupo hapa, kwani amefufuka kama alivyosema. Njoni, mpatazame mahali alipolazwa. Nanyi nendeni upesi, mkawaambie wanafunzi wake, Amefufuka katika wafu. Tazama, awatangulia kwenda galilaya; ndiko mtakakomwona. Haya nimekwisha waambia.” Mathayo  28:1-7

Roho Mtakatifu ni Nguvu ya Mungu na ni Pumzi ya Mungu yenye kuleta uhai tena. Kama Kristo alihamishwa toka kwa wafu nasi tutahamishwa kiroho na kimwili kwa nguvu za Roho Mtakatifu.

ROHO MTAKATIFU UFUNGUA VIFUNGO VYA UTASA;
Kwa nguvu za Roho Mtakatifu na uweza wake Sara alipokea uwezo wa kuwa na mimba alipokuwa amepita wakati wake. Milango na malango ya utasa yaliyomfunga Sara muda wa miaka wa ishirini na mitano, kwa imani ilifunguliwa.
Kwa imani hata Sara mwenyewe alipokea uwezo wa kuwa na mimba; alipokuwa amepita wakati wake; kwa kuwa alimhesabu yeye aliyeahidi kuwa mwaminifu.Waebrania 11:11
Hata sasa  kwa uwezo wa nguvu za Roho Mtakatifu, wako wakristo wengi watafunguliwa ndani mwa maombi ya kufungua milango na malango ya UTASA yasiwafunge tena maana yeye aliyeahidi ni mwaminifu na kusema, hatakuwepo mwenye kuharibu mimba wala aliye tasa katikati yetu.

Roho Mtakatifu akufunike kama kivuli wewe uliyekuwa umefunikwa na roho chafu za mashetani. Roho Mtakatifu na nguvu zake zikufunike kama kivuli, ili Vuli la uchawi na uganga litoke kwako. Kwa nguvu za Roho mtakatifu tumevishwa uweza na Kristo Yesu wa kufungua na kufunga na tutakachokifungua kitafunguliwa katika Mungu aliye hai. Na tutakachokifunga kitafungwa katika Mungu aliye hai. Maana maandiko yanasema;
 “Na ufungua wa nyumba ya Daudi nitauweka begani mwake; yeye atafungua wala hapana atakayefunga; naye atafunga wala hapana atakayefungua.” Isaya 22:22

Nguvu zake Roho mtakatifu zitakapokufunika, Utatenda makuu kwa uwezo wake. Katika yeye Roho Mtakatifu, Wagonjwa wanapokea uponyaji, wanaosumbuliwa na nguvu za mapepo wanawekwa huru mbali na mateso, walioshushwa chini na kudharauliwa wanainuliwa tena. “Akawaita wale Thenashara, akawapa uwezo na mamlaka juu ya pepo wote na kuponya maradhi.” Luka  9:1

Ni lazima tuhamishwe kwa Maombi yenye Imani. Usikubali kuteswa na kugandamizwa, Mtwike Yesu fadhaha zako, mizigo yako, taabu zako, vilio vyako  naye atakuhamisha tu.  Bwana atazitangua ishara zao wachawi na waganga, Maana kwa nguvu za Roho Mtakatifu hakuna uchawi wala uganga kusimama mbele yako tena. BWANA wa majeshi anasema; “Hakika hapana uchawi juu ya Yakobo, Wala hapana uganga juu ya Israeli.” Hesabu 23:23

Ushuhuda wa dada mmoja
Dada mmoja toka pale Kilimanjaro; alinijia akiwa na mateso ya magonjwa yaliyomkumba alipopigwa na upepo njia panda akiwa anakwenda dukani pale kijijini kwao. Baada ya kupigwa na upepo alianguka na kuzimia, alipozinduka alijikuta yuko hospitali akiwa amelazwa. Baada ya miaka miwili kupita tangu apigwe na upepo wa ajabu, ndipo alipokuja kwenye Ibada ya Maombezi ya kufungua Milango na Malango. Ndipo nilipomwombea kwa kuziita nguvu za Roho mtakatifu zenye kung’oa kila aina ya  mapando yaliyopandikizwa kwa watu wa Mungu. Hapa tunaona wachawi wanatumia upepo kumloga na kumwingia dada huyu. BWANA anatuma nguvu ya Roho mtakatifu katika kanisa la kwanza kama uvumi wa upepo. Maandiko yanathibitisha kwamba; “Hata ilipotimia siku ya Pentekoste walikuwako wote mahali pamoja. Kukaja ghafula toka mbinguni uvumi kama uvumi wa upepo wa nguvu ukienda kasi, ukaijaza nyumba yote waliyokuwa wameketi. Kukawatokea ndimi zilizogawanyikana, kama ndimi za moto uliowakalia kila mmoja wao.” Matendo ya Mitume 2:1-4

Upepo wa kichawi na kiganga uliokuwa unamtesa huyu dada ulimalizwa nguvu zake na kubatilishwa kwa Nguvu za Upepo wa Roho Mtakatifu, nikatengua kila aina ya upepo mchafu ulio mpitia kwa jina la Yesu Kristo.









Mpendwa msomaji bado naendelea na somo hili la MAOMBI YA KUFUNGUA MALANGO NA MILANGO na ninapenda kukutaarifu ya kuwa KITABU  cha somo hili tayari kipo mtaani hvy fika katika kanisa la EAGT City Center ili ujipatie nakala ya kitabu chako. 

UFUNGUO WA NNE

MAOMBI
Maombi:  maana yake ni kusemezana na MUNGU au kutafuta uso wa BWANA; katika hali ya unyenyekevu na kicho “Toka mbinguni BWANA aliwachungulia wanadamu, AONE KAMA YUKO MTU mwenye akili, Amtafutaye Mungu.” Zaburi 13:2
Katika kipengele hiki tunakwenda kujifunza maombi kama ufunguo wa kufungua milango na malango yaliyofungwa.
 “BWANA akamtokea Sulemani usiku, akamwambia, Nimesikia uliyoyaomba, na mahali hapa nimejichagulia kuwa nyumba ya dhabihu. Nikizifunga mbingu isiwe mvua, tena nikamuru nzige kula nchi, na nikiwapelekea watu wangu tauni; ilkiwa watu wangu walioitwa kwa jina langu, watajinyenyekesha, na kuomba, na kunitafuta uso, na kuziacha njia zao mbaya; basi nitasikia toka mbinguni, na kuwasamehe dhambi yao, na kuponya nchi yao. Sasa macho yangu yatafumbuka, na masikio yangu yatasikiliza maombi ya watu waombao mahali hapa. Maana sasa nimeichagua nyumba hii na kuitakasa ili kwamba jina langu lipate kuwako huko milele; yatakuwako na macho yangu, na moyo wangu daima. 2Mambo ya Nyakati 7:12-16

Tunajifunza kwa mfalme Sulemani jinsi alivyo jinyenyekeza na kusimama madhabahuni pa BWANA ikiwa ni ishara iliyowazi ya kuwa BWANA ndiye mfalme wa wafalme astahiliye kuabudiwa na kutukuzwa. Hivyo tunajifunza mambo manne yafuatayo:-
(1) “Ikiwa watu wangu watajinyenyekesha” watu wa Mungu lazima watambue ushindi wao dhidi ya malango ya giza unapatikana ndani mwa maombi sio nje ya maombi. Mtu akijinyenyekesha sawasawa na Neno la Mungu hakika atashinda na zaidi ya kushinda. “… Ikawa, Musa alipoinua mkono wake, Israeli walishinda; na aliposhusha mkono wake Amaleki walishinda. Lakini mikono ya Musa ilikuwa mizito; basi wakatwaa jiwe, wakaliweka chini yake akalikalia. Haruni na Huri wakaitegemeza mikono yake, mmoja upande huu na mmoja upande huu; mikono yake ikathibitika hata jua lilipokuchwa Yoshua akaangamiza amaleki na watu wake kwa ukali wa upanga…” Kutoka 17:8-16
Kwa kuinua mikono yake kwa BWANA Musa anaonyesha wazi jinsi anavyomtumaini na kumwamini Mungu. Waamaleki walipotokea kupigana na Israeli lengo lao ni kuwazuia wasipite walifunga malango na milango kwa njia ya kuanzisha vita. Nguvu ya ushindi ya Israeli ilitegemea kudumu katika Maombi, Imani na utii kwa Mungu. Wakati maombi ya Musa yalipokoma (aliposhusha mikono) mtililiko wa nguvu za Mungu ulikoma kwa watu wa Mungu. Hii ikiwa dhahiri kwamba tunapoomba nguvu ya Mungu hushuka na kinyume chake tusipoomba hakuna nguvu ya Mungu inayoshuka. 

Pia tunajifunza ya kwamba Baraka za Mungu na Ulinzi wa Mungu havishuki hivhivi kwetu mpaka tuvishushe kwa njia ya Maombi. “Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa; kwa maana kila aombaye hupokea naye atafutaye huona naye abishaye atafunguliwa.” Mathayo 7:7-8

(2) “Na Kuomba” maana yake, watu wa Mungu lazima waombe kwake bila kukoma kwa ajili ya kupata rehema na neema zitokazo kwa Mungu na lazima wamtegemee moja kwa moja na kumwamini yeye aingilie kati. Bwana Yesu Kristo anasema; “…imewapasa kumwomba Mungu siku zote, wala wasikate tamaa.”
Luka 18:1-
Katika maisha ya imani yako mapito mbalimbali yenye magumu, vita, dhiki, njaa, magonjwa na adha mbalimbali ambazo mtu wa Mungu anakabiliana nazo (changamoto za maisha). Pamoja na changamoto zote hizi hatukati tamaa bali tunatiwa nguvu katika yeye Kristo Yesu. Maandiko matakatifu yanasema “Kwa hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa n je unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku. Maana dhiki yetu nyepesi iliyo ya muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele uzidio kuwa mwingi sana; tusiviangalie vinavyoonekana bali visivyoonekana. Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu; bali visivyoonekana ni vya milele.” 2Wakorintho 4:16-18

(3) “Kutafuta uso wa Mungu” Watu wa Mungu ni lazima wamrudie Mungu kwa bidii na kwa moyo wote na kutamani uwepo wake na sio tu kujaribu kukimbia shida ndipo milango yao na malango yao yatakapofunguliwa siku zote za maisha yao. Katika maisha ya huduma ya Yesu Kristo hapa duniani aliutumia ufunguo huu wa kuutafuta uso wa Mungu aliye hai na maombi yake yalisikiwa na uweza wa Mungu ulikuwa ukimtoka na kuponya watu. Alianza kwa maombi (Luka 4:1-14), akadumu katika maombi (Luka 6:12-19)  na kumalizia katika maombi (Luka 22:39-46).  Tofauti sana na maisha ya wakristo walio wengi ambao huomba wakati wa shida na majaribu.  “Yeye, siku hizo za mwili wake, alimtolea yule, awezaye kumwokoa na kumtoa katika mauti, maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu; na ingawa ni mwana, alijifunza kutii kwa mateso hayo yaliyompata; naye alipokwisha kukamilishwa, akawa sababu ya wokovu ya milele kwa watu wote  wanao mtii; kisha ametajwa na Mungu kuwa kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki” Waebrania 5:7-10

(4) “Kuziacha njia zao mbaya” Watu wa Mungu ni lazima watubu kwa kweli ya Mungu na kuziacha njia zao mbaya ndipo maombi yao na dua zao zitasikiwa. Bwana Yesu Kristo alisema “… amin, amin, nawaambia, kila atendaye dhambi ni mtumwa wa dhambi. Wala mtumwa hakai nyumbani siku zote; mwana hukaa siku zote. Basi mwana akiwaweka huru mtakuwa huru kwelikweli.” Yohana 8:34-36

Hivyo BWANA anataka kabla ya mambo yote katika maisha yetu tufanye maombi kwa sababu ndiyo ufunguo unaofungua njia. Pasipo kufungua milango na malango kwanza hatuwezi kupenya kiroho na kimwili. Tukisoma maandiko matakatifu yanaonyesha dhahiri hakuna mtu wa Mungu aliye shinda pasipo maombi tangu baba zetu wa imani mpaka manabii walishika sana ufunguo huu wa maombi. “Basi, kabla ya mambo yote, nataka dua, na sala, na maombezi, na shukurani, zifanyike kwa ajili yua watu wote; kwa ajili ya wafalme na wote wenye mamlaka, tuishi maisha ya utulivu na imani, katika utauwa wote na ustahivu. Hili ni zuri, nalo lakubalika mbele za Mungu Mwokozi wetu; ambaye hutaka watu wote waokolewe, na kupata kujua yaliyo kweli. Kwa sababu Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu; ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote, utakaoshuhudiwa kwa majira yake.” 1Timotheo 2:1-6

Haya ni Maombi yenye kujengwa katika Msingi wa Neno la Mungu,
Imani itokanayo na Neno la Mungu. Mwombaji ni lazima Aombe sawa sawa na Neno la Mungu.

Yesu baada ya kubatizwa kabla ya Huduma alianza kwa Maombi, ambayo yalifanya mbingu zimfungukie. Kwa mantiki hiyo tunajifunza yakuwa Maombi ufungua malango na milango ya mbingu. Tunaona mfano wa Kristo Yesu kama kielelezo; 
“Ikawa, watu wote walipokwisha kubatizwa, na Yesu naye amebatizwa, naye anaomba, mbingu zilifunuka; Roho Mtakatifu akashuka juu yake kwa mfano wa kiwiliwili, kama hua, sauti ikitoka mbinguni, Wewe ndiwe Mwanangu, mpendwa wangu, nimependezwa nawe.” Luka 3:21-22

Katika maisha yetu ya ukristo tukitaka kufungua milango na malango kwa ajili yetu wenyewe, kwa ajili ya watoto wetu, kwa ajili ya mali zetu sharti tutumie kwa bidii ufunguo huu wa Maombi, sawasawa na ushahidi wa Neno la Mungu lilivyonenwa kwa kinywa cha mtumishi wa Mungu Ezra alipokuwa anaongoza watu wa Mungu toka uahamishoni Babeli kwenda kujenga na kufungua milango na malango ya Yerusalemu. pamoja na kuwa na kilakitu cha kujengea kama vile dhahabu, fedha na vitu vingi vya thamani. Ezra hakuvitegemea hivyo bali aliutegemea mkono wa BWANA ulio hodari ndio maana aliitisha mbiu ya kufunga na kuomba ili kujitafutia njia iliyonyooka itokayo kwa Mungu kabla ya kuanza safari. Ndipo nikaamuru kufunga, hapo penye mto Ahava, ili tupate kujinyenyekeza mbele za Mungu, na kutafuta kwake njia iliyonyoka, kwa ajili yetu sisi wenyewe, na kwa ajili ya watoto wetu, na kwa mali yetu yote. Maana naliona haya kumwomba mfalme kikosi cha askari na wapanda farasi, ili kutusaidia juu ya adui njiani, kwa maana tulikuwa tumesema na mfalme, tukinena, Mkono wa Mungu u juu ya watu wote wamtafutao, kuwatendea mema; bali uweza wake na ghadhabu yake ni kinyume cha wote wamwachao. Basi tukafunga, tukamsihi Mungu wetu kwa ajili ya hayo; naye akatutakabali.” Ezra  8:21-23

Yako mema toka kwa Mungu aliye hai kwa Mwombaji. MBINGU ZIKIFUNGUKA ndani mwa Maombi, Magonjwa yataondoka katika miili ya watu, Maana Maombi hushusha Uweza wa Ki-Mungu wenye nguvu ya kufungua Mafungo yote. Yesu Kristo baada ya Kuomba, Mbingu zilifunguka, kilichotokea ni Udhihirisho wa nguvu za Ki-Mungu zenye kuponya watu.

“Lakini yeye alikuwa akijiepua, akaenda mahali pasipokuwa na watu, akaomba. Ikawa siku zile mojawapo alikuwa akifundisha, na Mafarisayo na waalimu wa torati walikuwa wameketi hapo, waliotoka katika kila kijiji cha Galilaya, na Uyahudi, na Yerusalemu, na uweza wa Bwana ulikuwapo apate kuponya.” Luka  5:16-17

UWEZA WA BWANA ndio unaofungua Malango na Milango kwa Mwombaji. Pasipo Maombi hakuna kitakacho tendeka katika maisha ya mkristo anaye mtegemea Mungu. “Ikwa siku zile aliondoka akaenda mlimani ili kuomba, akakesha usiku kucha katika kumwomba Mungu. Hata kulipokuwa mchana aliwaita wanafunzi wake, akachagua kumi na wawili miongoni mwao, ambao aliwaita mitume, Simoni, aliyemwita jina pili, Petro na Andrea nduguye, na Yakobo na Yohana, na Filipo na Bartolomayo, na Mathayo na Tomaso, na Yakobo wa Alfayo, na Simon aitwaye Zelote, na Yuda wa Yakobo, na Yuda Iskariote, ndiye aliyekuwa msaliti. Akashuka pamoja nao, akasimama mahali tambarare, pamoja na wanafunzi wake wengi, na makutano makubwa ya watu waliotoka Uyahudi wote na Yerusalemuu, na Pwani ya Tiro na Sidoni, waliokuja kumsikiliza na kuponywa magonjwa yao na wale waliosumbuliwa na pepo wachafu waliponywa. Na makutano yote walikuwa wakita kumgusa, kwa sababu uweza ulikuwa ukimtoka ukiwaponya wote.” Luka  6:12-19

Yesu Kristo, anafanya Maombi usiku kucha maana yake anakesha katika Maombi. Matokeo yake ni Udhihirisho wa nguvu na uweza wa ki-Mungu unashuka kwa watu na kuwaponya. Ndani mwa maombi ndimo tunamovishwa Uweza na Nguvu za ki-Mungu aliye hai zenye kuangusha malango na ngome za kuzimu.

Yesu Kristo alikuwa na uwezo katika Kutenda na Kunena, lile Neno alilolisema kwa watu liliambatana na Uwezo na Nguvu. Maana wako watumishi wengi wa Mungu ambao wananena tu lakini neno lao halina nguvu matokeo yake kondoo wa BWANA wanaingia na mizigo yao kwenye ibada na wanatoka na mizigo yao. Kukosa funguo za ufalme wa Mungu ni jambo la hatari kwa mtumishi wa Mungu.

Unapomwendea Mungu sharti ujue unasimamia Neno gani la Mungu, maana Mungu hulituma Neno na ndani yake ndimo ulimo Uzima. Katika maisha yetu ya wokovu tunaweza kukutana na watu wengi wenye wivu na nia ovu, kama hawa makuhani wa kisadukayo kwa wivu wao waliwakamata mitume wakawatupa gerezani lakini kwa mkono wa BWANA wenye nguvu alituma malaika wake akawafungua mafungo yao;  sawasawa na Neno la Mungu. Toka kitabu cha Matendo ya Mitume 5:18-20 Neno linasema; “Wakawakamata mitume wakawaweka ndani ya gereza, lakini malaika wa Bwana akafungua milango ya gereza usiku, akawatoa, akasema, Enendeni mkasimame hekaluni mkawaambie watu maneno yote ya Uzima huu.”  

Hapa tunajifunza ya kuwa hatuko peke yetu katika mapito yetu yuko asiyeshindwa. Wajapofunga magereza yao, wajapofunga ndoa zetu, wajapofunga watoto wetu wasiolewe, wajapofunga uchumi wetu yatupasa tumwite Mungu aliye hai naye hakika atatufungua maana kwa msaada wa BWANA tutatenda makuu, na maadui zetu tutawakanyaga kwa nguvu zake. Japo gereza liliendelea kulindwa na walinzi na malango yake na milango yake kufungwa BWANA aliposhuka ndani ya gereza alifanyika mlango wa kutokea.  “Hata watumishi walipofika hawakuwaona gerezani, wakarudi wakatoa habari, wakisema, gereza tumeikuta imefungwa salama, nao walinzi wamesimama mbele ya mlango; lakini tulipoufungua hatukukuta mtu ndani.” Matendo 5:22-23

Kila kilicho kamatwa kikawekwa ndani ya Gereza la Kiganga na Kichawi, gereza la magonjwa, gereza la nyumba ndogo, gereza la kuzaa kufa kufa na mapooza, gereza la kufeli katika masomo/ kutokufaulu katika mitihani, gereza la uchumi, Lazima VITAFUNGULIWA.

 “Basi watu wote wakulao wataliwa, na adui zako wote watakwenda kufungwa, kila mmoja wao, na hao walio kuteka nyara watatekwa, na wote waliokuwinda nitawafanya kuwa mawindo. Maana nitakurudishia afya, nami nitakuponya jeraha zako, asema BWANA” Yeremia  30:16-17

BWANA akufungulie Mlango na Milango sawa sawa na Kuomba kwako. Mungu analiangalia Neno lake apate kulitimiza, hivyo Omba sawa sawa na Neno utapata jawabu lako. Usiogope, Maana hutapatwa na aibu tena; Tunayo mamlaka ya kugeuza kila hali sawasaw na Neno la Mungu alilonena kwa kinywa cha nabii Isaya na kusema; “Nimeziona njia zake; nami nitamponya, nitamwongoza pia, nitamrudishia faraja zake, yeye na hao wanaomlilia.” Isaya  57:18

Maombi yanafungua Malango na Milango ya Mbingu. Naye BWANA humwongoza daima mtu Mwombaji na Kuishibisha nafsi yake mahali pasipokuwa na maji na kumtia nguvu. Sawasawa na Neno la Mungu lililonenwa na kinywa cha nabii Isaya“Naye BWANA atakuongoza daima, ataishibisha nafsi yako mahali pasipokuwa na maji, na kuitia nguvu mifupa yako; nawe utakuwa kama bustani iliyotiwa maji, na kama chemchemi ambayo maji yake hayapungui.” Isaya  58:11

AYUBU aliomba Ustawi kwa ajili yake, kwa ajili ya watoto wake na mali zake. Akatoa Sadaka za kuinuliwa mbele za Mungu aliye hai akiziambatanisha na Maombi yake. Naye BWANA akamwitikia na kumstawisha katika hayo aliyoyaomba na kuyatolea sadaka.

 “Basi ilikuwa, hapo hizo siku za karamu zao zilipokuwa zimetimia, Ayubu hutuma kwao akawatakasa, kisha akaamka asubuhi na mapema, na kusongeza sadaka za kuteketezwa kama hesabu yao wote ilivyokuwa; kwani Ayubu alisema, Yumkini kwamba hawa wanangu wamefanya dhambi, na kumkufuru Mungu mioyoni mwao. Ndivyo alivyofanya Ayubu sikuzote. Ilikuwa, siku moja ambayo hao wana wa Mungu walikwenda kujihudhurisha mbele za BWANA, Shetani naye akaenda kati yao. BWANA akamwuliza Shetani, Umetoka wapi wewe? Ndipo Shetani akamjibu BWANA, na kusema, Natoka katika kuzunguka-zunguka duniani, na katika kutembea huku na huku humo. Kisha BWANA akamwuliza Shetani, Je! Umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu? Kwa kuwa hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu. Ndipo Shetani akamjibu BWANA, na kusema, je! Huyo Ayubu yuamcha BWANA bure? Wewe hukumzingira kwa UKINGO pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? Kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi.” Ayubu 1:5-10
Katika fungu hili la Neno la Mungu tunapata kielelezo cha mtu wa imani, mchaji wa Mungu, mwelekevu na aliyejiepusha na uovu. Tunapata taswira ya maisha yake ya kiimani jinsi alivyo yajenga katika msingi wa maombi, hata wakati wa mapito yake BWANA aliendelea kuwa Ukingo kwake. Ndiyo maana alisema “Lakini mimi najua ya kuwa Mteteaji wangu yu hai, nay a kuwa hatimaye atasimama juu ya nchi. Na baada ya ngozi yangu kuharibiwa hivi, lakini, pasipokuwa na mwili wangu nitamwona Mungu; nami nitamwona mimi nafsi yangu, na macho yangu yatamtazama wala si mwingine…” Ayubu 19:25-27 

Ayubu alifanya maombi maalumu kwa ajili ya watoto wake hakuwaacha wajiendeendee bali alisimama kama kuhani wa familia yake, akawainua mbele za Mungu kwa maombi na sadaka. Nasi katika maisha yetu tumepewa ukuhani usioondoka katika Kristo Yesu. Yatupasa kusimama imara katika maombi kuyafungua malango na milango, kwa ajili yetu sisi, watoto wetu na mali zetu. Kwa kuwa Mungu anamtafuta mtu miongoni mwetu atakayesimama mbele zake mahali palipo bomoka na kujenga boma. “Nami nikatafuta mtu miongoni mwao, atakayelitengeneza boma, na kusimama mbele zangu mahali palipobomoka, kwa ajili ya nchi nisije nikaiharibu, lakini sikuona mtu.” Ezekieli 22:30



Total Pageviews

Eagt City Centre Blog 2013. Powered by Blogger.

About Me

My photo
Jicho langu latoka machozi lisokome,wala haliachi;Hata BWANA atakapoangalia. Nakutazama toka mbinguni Maombolezo 3:49-50

Followers

Featured Posts

Popular Posts

Recent Posts

Text Widget